Alhamisi, 14 Mei 2015

Hatma ya Rais Nkurunziza Bado Haijulikani.....Baraza la Usalama la UN Laitishwa kwa Dharura, Marekani Yasema Bado Inamtambua Nkurunzinza kama Rais


Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa linatarajiwa kufanya mkutano wa dharura hii leo kuijadili Burundi baada ya jenerali mwandamizi wa jeshi nchini humo kutangaza kumpindua Rais Pierre Nkurunzinza kutoka madarakani. 
 
Ufaransa ndiyo imeitisha kikao hicho cha dharura ambacho kitafanyika hii leo punde tu baada ya wanachama wa baraza hilo la usalama la Umoja wa Mataifa kuijadili Iraq.
 
Hapo jana Meja Jenerali Godefroid Niyombare ambaye alikuwa mkuu wa shirika la ujasusi nchini Burundi, alitangaza kuwa utawala wa Rais Pierre Nkurunzinza umepinduliwa na jeshi kutoka madarakani kwa kukiuka matakwa ya raia.
 
Wakati wa tangazo hilo la kupinduliwa kwa serikali, Nkurunzinza alikuwa Tanzania kuhudhuria mkutano wa viongozi wa jumuiya ya nchi za Afrika Mashariki uliotishwa na mwenyekiti wa jumuiya hiyo Rais wa Tanzania Jakaya Kikwete kuujadili mzozo huo wa Burundi.

Niyombare aliagiza viwanja vyote vya ndege na mipaka yote ya ardhini ya Burundi kufungwa. Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon ametoa wito wa dharura kwa pande zote nchini Burundi kuonyesha utulivu na kujizuia kufuatia jaribio la mapinduzi ya serikali dhidi ya Rais Nkurunzinza.
 
Msemaji wa katibu huyo mkuu wa Umoja wa Mataifa Stephanie Dujarric amesema Ban amesisitiza haja kwa viongozi wote wa Burundi kudumisha amani na uthabiti katika taifa ambalo limekumbwa na matukio ya ghasia mbaya katika kipindi cha nyuma.
 
Marekani imewataka waburundi kuweka silaha chini kufuatia ripoti za kupinduliwa kwa serikali ya Nkurunzinza na msemaji wa ikulu ya Rais wa Marekani Josh Ernest amesema nchi yake inafuatilia matukio yanavyojiri Burundi kwa makini na wasiwasi.
 
Marekani imesema bado inamtambua Nkurunzinza kuwa kiongozi rasmi wa Burundi lakini inamshinikiza kuheshimu katiba ya taifa hilo na mikataba ya amani ilyofikiwa mwaka 2000 kwa kutogombea muhula wa tatu.
 
Hatma ya Nkurunzinza haijulikani baada ya ofisi ya Rais hapo jana kutangza anarejea nyumbani kutoka mkutano wa viongozi wa Afrika Mashariki nchini Tanzania na alitarajiwa kulihutubia taifa.
Lakini ndege yake haikuweza kutua mjini Bujumbura na  badala  yake  ilirudi  Tanzania  baada ya viwanja vya ndege kufungwa.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni